Friday, September 16, 2011

Mama Maria atoa pole kwa maafa Zanzibar

 Na Grace Michael, Butiama
MAMA Maria Nyererea ambaye ni Mjane wa Baba wa Taifa, ametoa pole kwa Taifa na kuonesha masikitiko yake juu ya maafa yaliyotokea mwishoni mwa wiki iliyopita yaliyosababishwa na ajali za kuzama kwa Meli ya Mv Spice Islanders katika Mkondo wa Nungwi.
 
Mbali na maafa hayo makubwa, pia Mama Maria ametoa pole kwa waliofikwa na maafa yaliyotokana na kupasuka kwa bomba la mafuta jijini Nairobi Kenya ambapo mamia ya watu walipoteza maisha.
Mama Maria aliyasema hayo juzi nyumbani kwake Butiama wakati akizungumza na baadhi ya waandishi waliomtembelea kwa lengo la kumjulia hali na kuzulu kaburi la Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
“Kwa kweli natoa pole kwa Taifa zima kutokana na msiba mzito uliotokea huko Zanzibar lakini na kwa Afrika Mashariki nzima...ni msiba mzito sana,” alisema Mama Maria.
 
Akizungumzia afya yake, alisema ni njema na anafarijika kuona watu wakizulu makazi ya baba wa Taifa na kwa lengo la kumjulia hali yeye mwenyewe.
“Mimi afya yangu ni nzuri sijui wengine...lakini kwa upande wangu ni mzima kabisa, nimefarijika sana kunitembelea kwani nikiona hivi nafurahi sana,” alisema.
Alieleza kufurahishwa na kufarijika kutokana na hatua Watanzania kumtembelea mara kwa mara ili kumjulia hali nyumbani kwake.
“Wakati mwingine si jambo rahisi kwa watu kukutembelea kila mara wakati si mtumishi wa serikalini, ni mstaafu.Wapo watumishi wa serikali ambao baada ya kustaafu hawapati bahati ya kutembelewa na wananchi, hii ni bahati na inanifariji sana,” alisema Mama Maria
Meli ya Mv Spice Islanders ilizama katika Mkondo wa Nungwi, alfajiri ya kuamkia Septemba 10, mwaka huu ilipokuwa safarini kutoka Kisiwa cha Unguja kwenda kisiwani Pemba
Katika tukio la kupasuka kwa bomba la mafuta katika Jiji la Nairobi, watu zaidi ya 100 wameripotiwa kufa na wengine kujeruhiwa vibaya kutokana na bomba hilo kulipuka moto na kuwateketeza watu walikuwa wakichota mafuta yaliyokuwa yakitiririka.
Mama Maria alisema Watanzania na watu wa Afrika Mashariki wapo katika masikitiko makubwa kutokana na vifo vya ndugu, jamaa na marafiki zao vilivyosababishwa na matukio ya ajali hizo mbili.
 

Thursday, September 8, 2011

Wahandisi wataka kujitosa kumaliza tatizo la umeme


Na Grace Michael

BODI ya Usajili ya Wahandisi (ERB), imesema tatizo la umeme linaloikabili nchi kwa sasa lisingefika hapo lilipo endapo serikali ingewashirikisha wataalam hao katika hatua mbalimbali.

Kutokana na hali hiyo, wameiomba serikali kuhakikisha inatoa ushirikiano wa kutosha katika mambo mbalimbali yanayohusu fani hiyo, ili kuepukana na matatizo kama tatizo la umeme kwa sasa.

Akitoa salamu za bodi hiyo wakati wa kufunga wa mkutano uliokutanisha bodi tatu za sekta ya ujenzi, Bw. Gema Modu, alisema kuwa; “Kungekuwa na ushirikishwaji wa uhakika katika suala la umeme, suluhu ingekuwa imepatikana, hata tatizo hili lisingefikia hapo lilipo,”

Aliongeza kuwa; “Tatizo hili la umeme kwa upande wetu tunalichukulia kwa sura mbili moja ikiwa ni tatizo na nyingine ni fursa kwetu ya kuingia kufanya kazi hiyo na katika hili tumejipanga na tutaingia huko kwa lengo la kusaidia.”

Bodi nyingine zilizoshiriki mkutano huo ni pamoja na Bodi ya Wakandarasi (CRB), Bodi ya Wasanifu na Wakadiria majengo ambao kwa pamoja walijadili masuala mbalimbali ya sekta ya ujenzi na hatimaye kutoka na maamuzi ambayo yatawasilishwa serikalini kwa lengo la kuboresha sekta hiyo.

Mkutano huo ambao ulifungwa na Waziri wa Miundombinu Dkt. John Magufuli kwa niaba ya Makamu wa Rais Dkt. Mohamed Gharib Bilali, aliwataka wataalam hao kuwa wawazi katika mambo wanayotaka serikali iyafanyie kazi hata kama ni makali.

Andikeni mahitaji yenu kwa uwazi, msiwe wanasiasa katika kazi zenu...hata kama ni maneno makali andikeni na wenyeviti wa bodi waweke saini zao nami nitayapeleka kwa rais bila kuchakachua kitu chochote,” alisema Dkt. Magufuli.

Aidha aliwataka wote kwa pamoja kushirikiana katika kazi na kuachana na utamaduni wa kupigana vijembe na rushwa katika kazi na badala yake watangulize uzalendo katika shughuli zao kwa kuwa fani za ujenzi ndizo zenye mwelekeo wa maendeleo ya nchi, lakini pia ndizo zimeshikilia uchumi wa nchi.

Kwa mujibu wa hotuba ya Makamu wa Rais, serikali itazidi kuwashirikisha katika kazi za umma na kutoa upendeleo kwa wazalendo katika kazi hizo, lakini akaonya kuwa wasifanye kazi ambazo ziko chini ya kiwango.

Tunatambua kuwa kuna tatizo la mitaji na katika hili tunatoa mwito kwa mabenki kuwatazama kwa jicho la pekee wakati mnapojitokeza kuomba mikopo...suala la msingi ni kufanya kazi zenye viwango kwa kuwa serikali tunachefuliwa sana na majengo mabovu na kazi zote ambazo ziko chini ya kiwango,” alisema hotuba hiyo.

Alisema kuwa serikali inatambua madeni inayodaiwa na wataalam hao na ikaahidi kuwa sehemu kubwa ya madeni hayo italipwa hivi karibuni.



Hata hivyo washiriki wa mkutano huo wamekubaliana kupambana na tatizo la rushwa na wakashauri kuwepo mjadala wa wazi ambao utajadili suala hilo kwa uwazi na bila kuoneana aibu kwa kuwa rushwa ni ugonjwa unaoweza kuliua taifa.