Tuesday, March 27, 2012

Fedha za NHIF zinunulie dawa si kulipana posho-RC

Na Grace Michael, Mwanza

MKUU wa Mkoa wa Mwanza, Evarist Mbigiro amezitaka Halmashauri mkoani humo kuzitumia fedha zinazolipwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) katika ununuzi wa dawa na si kuzielekeza katika masuala mengine kama ya kulipana posho.

Amesema kuwa fedha hizo zimekuwa zikitumika katika matumizi ambayo hayakukusudiwa jambo linalokwamisha uboreshaji wa huduma za matibabu katika vituo vya kutolea matibabu.

Agizo hilo amelitoa katika mkutano wa wadau wa Mfuko huo uliofanyika leo jijini Mwanza na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo watoa huduma, wanachama, Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakuu wa Wilaya na wengine.

"Wenzetu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wanatulipa fedha lakini fedha hizo ndo utazikuta zinalipwa posho huku vituo vikikosa dawa...hili halikubaliki ni lazima tuone fedha hizi zikinunua dawa na wananchi wakipata tiba na kuwa na afya njema," alisema Mbigiro.

Alisema kuwa yeye kama Mkuu wa Mkoa atajisikia faraja kuona akiongoza wananchi wenye afya njema kwa kuwa watakuwa na uhakika wa kuzalisha na kukuza pato lao na la Taifa kwa ujumla.

Alisema kuwa inashangaza Mkoa kama wa Mwanza kuwa nyuma katika suala la wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) huku ukiwa na fursa nyingi za kiuchumi na pato la mwananchi wa Mwanza likikidhi mahitaji ya kujiunga na Mfuko huo ili kuwa na uhakika wa matibabu.

"Hapa tuna fursa nyingi zikiwemo za uvuvi, ufagaji, kilimo, madini, utalii na zingine na ili hizi fursa zitumike ni lazima wananchi hawa wawe na afya njema hivyo ni lazima tuhakikishe sisi viongozi tunawahamasisha wananchi wetu kwa kuwaeleza umuhimu wa kuwa na bima ya afya...sitakubali mkoa huu kubaki na asilimia 1.1 ya kaya zilizoko kwenye Mfuko wa CHF," alisema.

Kutokana na hali hiyo, alisema kuwa Uongozi wa Mkoa wa Mwanza utatoa ushirikiano kwa NHIF ili lengo la kuwafikia Watanzania asilimia 30 ifikapo 2015 lifanikiwe.

Aliongeza kuwa hata Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010 katika ibara ya 85 inasema wazi kuwa "Mandeleo ya Taifa letu yataletwa na wananchi wenye afya bora inayowezesha kuzalisha mali na kutoa huduma mbalimbali".

Mbigiro akitoa mwito kwa wanachama wa Mfuko huo, aliwataka kuwa walinzi wa huduma za Mfuko hasa wanapokutana na dawa zinazotolewa na Serikali zikiuzwa kwenye maduka binafsi.

Ili kutimiza lengo la kupanua wigo wa wanachama wa Mfuko huo, Mbigiro alizitaka Halmashauri kutunga sheria ndogo itakayowalazimu wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Emanuel Humba akitoa maelezo ya Mfuko huo kwa wadau, aliwataka watoa huduma kutumia fursa mbalimbali zinazotolewa na Mfuko huo ili kuboresha huduma za matibabu.
Aliahidi kuwa Mfuko utaendelea na juhudi za kutoa elimu kuanzia ngazi ya Taifa hadi ngazi ya kaya ili kuhakikisha lengo la afya bora kwa kila Mtanzania linafikiwa.

Tuesday, March 20, 2012

CHF italeta afya bora na kupunguza umasikini-Pinda

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda ameagiza Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) uwe agenda ya Kitaifa kwa kuwa ndio njia pekee ya kufikia lengo la Afya Bora kwa wote na kupunguza vifo na umasikini kwa Watanzania. 

Kutokana na umuhimu huo, ameiagiza Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kukaa na Uongozi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ili kuandaa mkakati utakaohakikisha Watanzania wote wanapata huduma za Mfuko huo kwa lengo la kuwawezesha kuwa na afya njema. 

Waziri Mkuu Pinda aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati wa maadhimisho ya miaka 10 ya NHIF tangu kuanzishwa kwake sherehe zilizofanyika Makao Makuu ya Mfuko huo. 

“Tunaweza kutumia uzoefu kutoka nchi mbalimbali ambazo zimepiga hatua katika masuala ya Bima ya Afya lakini kwa kuzingatia utamaduni na mazingira ya kitanzania, kampeni za uhamasishaji ziwe endelevu kwa viongozi wa Serikali, wawakilishi wa wananchi na viongozi wa dini…wote tushiriki katika kampeni hii tukizingatia kuwa suala hili linamhusu kila mtu,” alisema Pinda. 

Akizungumzia matumizi ya fedha za uchangiaji na uboreshaji wa Huduma, Fedha ambazo hulipwa na NHIF, alisema huelekezwa zaidi katika uboreshaji wa huduma nchini na mpaka sasa Mfuko huo umelipa zaidi ya sh. Bilioni 140 kwa vituo mbalimbali vilivyosajiliwa na Serikali, Mashirika ya Dini na binafsi.  

Hata hivyo alisema kuwa pamoja na fedha hizo kulipwa kwa lengo hilo, huduma bado si za kuridhisha hatua iliyomfanya kumwagiza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukagua matumizi ya malipo yatokanayo na uchangiaji wa huduma za afya zikiwemo za NHIF, tele kwa tele na papo kwa papo lengo ni kuhakikisha matumizi bora ya fedha za Mfuko na kutoa huduma bora zaidi. 

“Wito wangu hasa kwa watoa huduma, mjipange vizuri zaidi ili kuboresha huduma zenu, muwe waadilifu ili mpate malipo halali…msijihusishe na madai ya kughushi yatakayotishia uhai wa Mfuko wetu na msiruhusu kuharibu mahusiano yaliyo kati yenu na Mfuko, eleweni kwamba maendeleo ya Mfuko ndio mkombozi kwa wananchi wetu,” alisema Pinda. 

Pamoja na hayo, aliuopongeza uongozi wa Mfuko kwa kitendo cha kuwatambua waasisi wa Mfuko huo ambao wamesadia kuleta ufanisi na ustawi wa Mfuko hivyo akautaka kuendelea na utaratibu huo kwa kuwa unatoa hamasa kwa wengine kutoa mchango wao wa hali na mali katika kufanikisha malengo yaliyopo. 

Naye Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa katika salaam zake aliutaka Mfuko kulinda mafanikio yaliyofikiwa, kufanya kazi kwa bidii na maarifa huku wakijua kuwa bado kuna kundi kubwa la Watanzania wanaohitaji huduma hasa vijijini. 

‘Msiogope kuthubutu kufanya mambo yanayolenga  kuboresha huduma za matibabu kwa watanzania hasa katika ujenzi wa vituo vya matibabu, kusaidia vifaa tiba na elimu zaidi ili uhai wa Mfuko ubaki kuwa imara,” alisema Rais Mkapa. 

Aidha aliwataka wananchi kutodanganywa kuhusu afya zao hivyo suala la uchangiaji ni la muhimu na Bima ya Afya ndio mtindo wa sasa wa maisha.

MFUKO WA TAIFA WA BIMA YA AFYA ULIVYOADHIMISHA MIAKA 10















Add caption

Viongozi wakipata maelezo ya namna kumbukumbu zinavyotunzwa