Friday, October 12, 2012

NHIF yamuenzi kipekee Mwl Nyerere

Hayati Baba wa Taifa Mwl, Julius Nyerere

Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Emanuel Humba.
Na Grace Michael

KATIKA kuhakikisha Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage  Nyerere anaenziwa kipekee, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) unaendesha zoezi la upimaji afya za wanachama na wananchi kwa ujumla mkoani Shinyanga ambako kilele cha maadhimisho hayo yatafanyika Oktoba 14, mwaka huu.

Akizungumzia zoezi hilo, Mkurugenzi wa Uendeshaji Eugen Mikongoti alisema kuwa, Mfuko umefikia uamuzi huo kwa lengo la kuenzi mazuri yote yaliyofanywa na Baba wa Taifa enzi za uhai wake.

“Baba wa Taifa aliapa kupigana na maadui watatu ambao ni Umasikini, Ujinga na Maradhi na katika hayo sisi ni wadau wakubwa katika kupambana na adui maradhi na ndio maana tumeona tumuenzi kwa njia hii ambapo wananchi watapima afya zao bila malipo na kupata ushauri wa kitaalam ili kuepukana na maradhi yasiyoambukiza,” alisema Mikongoti.

Mbali na upimaji wa afya kwa wananchi, alisema kuwa Mfuko unatumia fursa hiyo kujibu kero mbalimbali za wanachama wake ambao watafika katika viwanja vya Sabasaba ambako Mfuko umeweka banda kwa ajili ya kuendesha zoezi la upimaji na utoaji wa elimu juu ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii, kwa muda wa siku tano, kuanzia jana.

Alisema kuwa lengo kubwa la NHIF ni kuhakikisha wanachama wake na wananchi kwa ujumla wanapata huduma bora za matibabu na Vituo vya kutolea huduma hizo vinaboreshwa kwa kuwa na vifaa vya kisasa vya uchunguzi kupitia fursa inayotolewa na Mfuko huo ya mikopo ya vifaa tiba na ukarabati wa majengo.

“Mfuko umekuwa na jitihada mbalimbali za kuhakikisha huduma za afya vituoni zinakuwa bora na unafanya hivyo kwa kutambua kuwa mhimili mkubwa wa Mtanzania katika kufanya kazi na kujiondolea umasikini ni afya yake kwanza…nawaomba wananchi wa Shinyanga na wa maeneo mengine mfike katika banda letu ambalo linatoa huduma za upimaji na elimu ya afya kwa ujumla,” alisema.

Mikongoti alisema kuwa Mfuko utaendelea kumuenzi Baba wa Taifa katika kupambana na adui maradhi kwa kuhakikisha Watanzania wanakuwa na uhakika wa matibabu kupitia utaratibu wa kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii.

Wakati huo huo, Mfuko umeendelea na jitihada zake za kuhakikisha makundi maalum yanapata huduma bora baada ya kuchangia jumla ya shilingi milioni 1.5, shuka 80 na fulana 80 kwa Kituo cha Mihuji Chesire Home kilichopo mjini Dodoma ambacho kinalea watoto wenye matatizo ya mtindio wa ubongo.

Mchango huo wa NHIF ulitolewa mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dodoma katika harambee ya kuchangia kituo hicho na Meneja wa Kanda ya Kati Dkt. Daudi Bunyinyiga ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo Emanuel Humba.

Akiwasilisha mchango huo, Dokta Bunyinyiga alisema kuwa Mfuko kama Taasisi inayofanya kazi na Jamii inawajibu wa kuhakikisha jamii inayoizunguka hususani watu wenye mahitaji maalum wanafaidika na huduma zake.

Ongezeni kasi ya uhamasishaji CHF-RC Lindi

Maandamano ya siku ya Afya ya Akili mkoani Lindi, wa tatu kutoka kulia ni Mwakilishi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Fortunatha Kulaya

Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Bw. Mwananzila akitia saini katika kitabu cha wageni kwenye banda la elimu la NHIF ambalo lilikuwa katika maadhimisho hayo, kushoto ni Meneja wa Kanda ya Mtwara, Joyce Sumbwe.


Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Mkoa wa Lindi, Ludovick Mwananzila amewataka viongozi mkoani humo kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkoa ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kuhakikisha wanaongeza kasi ya uhamasishaji wa wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ili wananchi wawe na uhakika wa kupata matibabu.
Rai hiyo aliitoa mapema wiki hii katika maadhimisho ya siku ya siku ya Afya ya Akili Duniani. Alisema “Hakikisheni kasi ya uhamasishaji inaongezeka na wanachi  wengi wanajiunga kwenye mfuko huu wa CHF, haiwezekani kwa mkoa wa Lindi uwe na  wanachama asilimia 5.4 % tu kati ya kaya 194,424,” alisema.
Katika maadhimisho hayo, Mfuko ulishiriki kikamilifu katika utoaji wa elimu ya namna ya kujiunga na utaratibu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii ambapo mpaka sasa mifuko hiyo inahudumia asilimia 18.7 ya Watanzania wote.
Hata hivyo Mkuu huyo wa Mkoa alitumia fursa kuwataka viongozi mkoani humo kuhakikisha wanajipanga katika kukabiliana na changamoto za huduma za matibabu  zilizopo kwenye mkoa hususani ya uhaba wa dawa katika vituo vya kutolea matibabu.
Kwa upande wa NHIF, akizungumzia maadhimisho hayo, Mwakilishi wa Mkoa wa Lindi,  Fortunata Kulaya alisema changamoto kubwa iko kwenye matumizi ya fedha zinazolipwa na mfuko huo hususan za tele kwa tele hivyo akaomba eneo hilo kuangaliwa kwa jicho la pekee ili fedha hizo ziweze kutumika katika matumizi yaliyokusudiwa.
 


Tuesday, October 2, 2012

NHIF yasogeza huduma, yazindua ofisi mpya tisa

Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mwantumu Mahiza akisisitiza jambo kwa uongozi wa NHIF kwenye uzinduzi wa ofisi mpya ya Mfuko huo iliyoko Kibaha.

Mkurugenzi Mkuu wa NHIF akitoa maelezo ya awali kabla ya uzinduzi wa Ofisi hiyo.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu Kibaha Dk. Mpemba akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa Mfuko katika uboreshaji wa huduma za matibabu.

Baadhi ya Maofisa wa Mfuko na wageni waalikwa wakisikiliza kwa makini

Wakibadilishana mawazo namna ya uboreshaji wa huduma za matibabu mkoani Pwani

Baadhi ya Wakurugenzi wa NHIF wakibadilishana mawazo kabla ya kuanza kwa hafla ya uzinduzi wa Ofisi hiyo.

Maofisa waliokuwa wakiandaa shughuli hiyo.



RC Mahiza aziundua ofisi mpya za NHIF

MKUU wa Mkoa wa Pwani, Bi. Mwantumu Mahiza ameutaka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuisaidia kwa hali na mali Hospitali ya Tumbi kutokana na umuhimu wake katika kuhudumia wagonjwa mbalimbali wakiwemo majeruhi wengi wa ajali zinazotokea katika maeneo ya mkoa huo.

Alisema kuwa kutokana na changamoto nyingi zinazoikabili Hospitali hiyo ikiwemo ya kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa kwa siku, ukosefu wa Vifaa vya kisasa vya uchunguzi, kuna haja kubwa kwa NHIF kuingilia kati ili kuinusuru hospitali hiyo na maisha ya Watanzania kwa ujumla.

Bi. Mahiza aliyasema hayo jana katika uzinduzi wa Ofisi mpya ya NHIF iliyopo mkoani Pwani ambayo iliwakilisha Ofisi zingine mpya nane zilizopo katika Mikoa ya Mara, Kigoma, Ruvuma, Rukwa, Singida, Lindi, Shinyanga, Kagera na Manyara ambazo zimefunguliwa na NHIF kwa lengo la kusogeza huduma kwa wanachama wake na kuboresha huduma kwa ujumla.

“Nimefarijika sana kwa kutupa heshima kubwa Mkoa wa Pwani, mngeeamua kwenda Mkoa mwingine kuzindua ili kuziwakilisha ofisi zingine, Niwaombe sana wenzangu NHIF, mtupe umuhimu wa kipekee katika kutusaidia vifaa tiba na hasa kifaa cha kutunzia damu salama, inashangaza na haieleweki kwa wasomi kama sisi kuona ajali na wagonjwa wakiwa Pwani na damu ikitunzwa Dar es Salaam...nakuagiza Mganga Mkuu wasilisha ombi hilo NHIF haraka iwezekanavyo,” alisema Mahiza.

Alisema kuwa suala la vifaa vya uchunguzi katika hospitali hiyo linamnyima usingizi kutokana na mazingira yanayoikabili hospitali hiyo ambayo kwa wastani inapokea wagonjwa 500 kwa siku.

Akijibu ombi hilo la Mkuu wa Mkoa, Mjumbe wa Bodi ya NHIF, Bi. Mwanaidi Mtanda alisema kuwa Bodi itahakikisha inatoa kipaumbele katika suala hilo kwa lengo la kuwezesha hospitali hiyo kuwa na vifaa vya kisasa ili huduma bora kwa wanachama na wananchi kwa ujumla zipatikane.

“Kwa niaba ya Bodi niseme kuwa Mfuko una nia ya dhati ya kusaidia Hospitali ya Tumbi na Mkoa wa Pwani kwa ujumla kwa lengo la kuboresha huduma na pale tutakapopokea maombi kutoka kwenu yatafanyiwa kazi haraka sana,” alisema Bi. Mtanda.

Bi. Mtanda hakusita kusema kuwa hamasa ya utumiaji wa fursa inayotolewa na NHIF ya utoaji wa mikopo ya vifaa tiba na ukarabati wa majengo kwa vituo hasa vya serikali bado ni mdogo hivyo akatumia fursa hiyo kuwaomba viongozi na wamiliki wa vituo vyote vya matibabu vilivyosajiliwa na Mfuko kuomba mikopo hiyo ili kuviwezesha vituo vyao kutoa huduma bora za matibabu.

Hata hivyo, Bi. Mwantumu alieleza wazi kuwa NHIF imekuwa chachu kubwa katika maendeleo ya sekta ya afya kutokana na ukweli kwamba vituo vingi vinaendesha shughuli zake kwa kutumia fedha zinazolipwa na Mfuko huo.

“Mtu yeyote anayefuatilia mwenendo wa Sekta ya Afya nchini atakubaliana nami nikisema Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, umekuwa chachu kubwa katika maendeleo ya sekta ya afya kwani kwa kiwango kikubwa vituo vingi vinaendesha shughuli zake kwa fedha zinazolipwa na Mfuko huo hivyo nawapongeza na kuwataka muendelee kusaidia,” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa NHIF, Bw. Emanuel Humba alisema kuwa lengo la uzinduzi wa ofisi hizo ni kutaka kuwajulisha wadau kuwa Mfuko umesogeza huduma zake karibu na wanachama ikiwa ni njia mojawapo ya uboreshaji wa huduma.

Alisema pamoja na Mfuko huo kukua kwa kasi na kuwa na mafanikio makubwa lakini bado unakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo za ukosefu wa dawa, vifaa tiba, upungufu wa wahudumu changamoto ambazo Mfuko unazifanyia kazi kupitia mipango mbalimbali ikiwemo ya kusajili maduka ya dawa muhimu na ukopeshaji wa vifaa tiba.

NHIF kwa sasa ina mtandao wa ofisi zake katika Mikoa yote Tanzania Bara na Zanzibar isipokuwa mikoa mipya.